Serikali na halmashauri wilayani Ngorongoro zimetakiwa kutoa ushirikiano
kwa redio za kijamii wilayani humo kwa lengo la kuwaletea maendeleo ya haraka wananchi wao.
Hayo yameelezwa na Meneja wa redio ya kijamii ya Loliondo FM, Joseph Munga, wakati wa ziara ya kukagua miradi inayoendeshwa na Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) redio hiyo ikiwa miongoni mwa miradi inayofadhiliwa na UNESCO wilayani hapa wakiambatana na wadau wa maendeleo kutoka kampuni ya Samsung na Ubalozi wa Uswiss hapa nchini.
Redio za Jamii ndio chombo pekee kinachoziunganisha serikali na jamii katika suala zima la kujiletea maendeleo alisema Joseph Munga.
Munga aliongeza kwa kusema kuwa redio hiyo iliyoanza kurusha matangazo mwezi Oktoba 2013 imekuwa ni kichocheo cha kutoa taarifa mbali mbali kwa jamii wilayani Loliondo na kuibua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii huku akiitaka serikali na halmashauri wilayani humo kuisaidia katika kufikia malengo ya kuitumikia jamii na kuwashukuru wadau mbali mbali wanaoiwezesha redio hiyo ikiwemo kampuni ya simu za mkononi ya Airtel ambayo imetoa mnara wao kurushia Matangazo ya redio Loliondo.
Suala hapa ni ushirikiano hasa kwa halmashauri kuelewa na kuona umuhimu wa kutumia redio hii katika matukio mbali mbali yanayofanyika kwenye halmshauri vikiwemo vikao vya baraza la madiwani ili wananchi walioshindwa kufika waweze kujua baraza lao limepitisha nini sanjari na huduma kwenye sekta za afya na elimu, alisema Munga.
Redio Loliondo ni miongoni mwa miradi inayofadhiliwa na UNESCO wilayani humo kupitia asasi isiyokuwa ya kiserikali ya RAMAT kwa kufadhili miradi ya Maktaba,kutoa elimu kwa jamii ya kifugaji yenye malengo ya kuinua uelewa na ufahamu kwa jamii hizo zilizopo pembezoni hasa katika suala zima la kujiletea maendeleo.
Nae Afisa Miradi ya Mawasiliano, Habari na Tehama wa UNESCO, Bw. Al Amin Yusuph, alisema kuwa misingi ya redio hiyo inalenga kuikomboa jamii ya Loliondo kwa kutoa elimu ya kifugaji na elimu kwa wananchi wilayani humo ambao hapo awali hawakupata fursa ya kupata taarifa na matukio mbalimbali yanayoendelea wilayani humo.
Akifafanua faida za redio hiyo kwa jamii ni kupata taarifa mbali mbali zinazoendana na shughuli zao za ufugaji hususan taarifa za chanjo ya mifugo na madawa na kupata taarifa nyingine kuhusiana na masuala mbali mbali ya kijamii ndani na nje ya wilaya hiyo ambayo hapo awali yalikuwa vigumu kupatikana kwa wakati kutokana na jiografia ya wilaya hiyo.
Pamoja na kwamba malengo ya mradi huu yameanza kuonekana dhahiri machoni petu,wafadhili kutoka UNESCO pamoja na kampuni ya simu za mikononi ya Airtel ambayo mnara wake umekuwa ukitumika kurusha matangazo ya redio hii, tunataka kuhakikisha kwamba mnaweza kujiendesha wenyewe hapo baadae ili mradi kama huu uweze kuwanufaisha na wenzenu sehemu zingine, alisema Al Amin.
Akizungumzia miradi inayoletwa na wafadhili wilayani humo Mkuu wa wilaya ya Ngorongoro, Elias Wawa Lali alisema kuwa imechangia kwa kiasi kikubwa kuwahamasisha vijana ambao wana shauku ya kuishi mijini kurudi nyumbani na kuendeleza jamii hali ambayo imetafsiriwa kutoa uelewa kwa wanajamii na hivyo ni faraja kubwa kwa wananchi wilayani Loliondo.
Ameyataka mashirika na taasisi za kiserikali na zisizo za kiserikali kuingalia Ngorongoro kwa ukaribu na kuwa wadau wazuri wa kuiletea maendeleo wilaya hiyo kwani miradi iliyopo itachochea ukuaji wa uchumi na kusaidia uelewa wa wakazi wilayani Loliondo katika dhana nzima ya kujileta maendeleo na kukuza uelewa wa wananchi wa kupata taarifa mbalimbali kwa wakati.